picha kutoka maktaba
SINGIDA -IKUNGI
NA Mwandishi wetu
Afisa
Mtendaji wa Kata (WEO) ya Sepuka, wilaya ya Ikungi mkoani Singida, Bahati Mkungile,
amewapongeza walimu na wazazi wa kata hiyo kwa jitihada kubwa walizozifanya
katika kuinua kiwango cha elimu na kuhakikisha wanafunzi wanafaulu masomo yao.
Pongezi hizo
zimetolewa baada ya wanafunzi 354 kutoka shule tano za msingi za Musimi,
Italala, Mnang`ana, Safina na Njaa kufaulu mtihani wa kumaliza elimu ya msingi
mwaka 2025 na kuanza masomo ya Kidato cha Kwanza mwaka 2026 katika shule za
sekondari za Msungua na Sepuka.
Bahati
Mkungile amesema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mzuri kati ya walimu,
wazazi na viongozi wa Serikali kutoka vijiji vya Musimi, Msungua na Mnang`ana,
ambavyo ndivyo vinamiliki shule hizo za msingi. Ameeleza kuwa ushirikiano huo
umejenga mazingira bora ya kujifunza na kuongeza hamasa kwa wanafunzi kuelewa
umuhimu wa elimu.
Akizungumza
ofisini kwake, Bahati alisema ongezeko la ufaulu ni matokeo ya bidii ya walimu
darasani, usimamizi wa karibu kutoka kwa wazazi pamoja na juhudi binafsi za
wanafunzi katika masomo yao.
Kwa upande
wake, Afisa Elimu Kata ya Sepuka, Iddi Kisuda, amesema jitihada hizo zimezaa
matokeo yanayohitajika na Taifa. Ameongeza kuwa endapo wazazi wataendelea
kushirikiana kikamilifu na walimu mwaka 2026, ufaulu utaongezeka zaidi kuliko
mwaka uliopita.
Kisuda pia ameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya
Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuboresha mazingira ya elimu
kupitia ajira za walimu wenye sifa, upatikanaji wa vifaa vya kufundishia, ujenzi
na ukarabati wa miundombinu ya shule pamoja na ujenzi wa nyumba bora za walimu.
Akitoa taarifa ya mapokezi ya wanafunzi, Mkuu wa Shule ya
Sekondari Msungua, Nossiah Bembela, amesema shule hiyo tayari imepokea
wanafunzi 185, huku 29 bado hawajaripoti. Amewahimiza wazazi kuhakikisha watoto
wao wanafika shuleni kwa wakati.
Naye Kaimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Sepuka, Mwalimu
Abubakari Amasi, amesema shule yake imepokea wanafunzi 105, huku 35
wakitarajiwa kuripoti. Amehimiza wazazi kuzingatia muda na taratibu za kuanza
masomo.
Mkazi wa Kijiji cha Msungua, Ramadhani Shabani Kiteu, amesema ufaulu huo umetokana na jitihada za walimu kupitia kambi za masomo, kuongeza muda na siku za ufundishaji kwa wanafunzi wa darasa la saba kwa kushirikiana na wazazi.





0 Comments