SINGIDA
Mbunge wa Jimbo la Ikungi Mashariki, Mhe. Thomas Mghonto
(Chief), ametembelea na kujionea zoezi la kliniki ya msaada wa kisheria
lililozinduliwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Homera, katika
viwanja vya Ukumbi wa RC Mission, Manispaa ya Singida.
Akiwa katika ziara hiyo, Mhe. Mghonto alimpongeza Waziri
Dkt. Homera kwa uamuzi wa kufika mkoani Singida na kuleta huduma ya msaada wa
kisheria kwa wananchi, akieleza kuwa ukosefu wa elimu ya sheria umekuwa
changamoto na kero kubwa kwa wananchi wengi, hususan wale wa kipato cha chini.
Mbunge huyo alisema kuwa wananchi wengi wamekuwa wakipoteza
haki zao kutokana na kutokujua misingi ya kisheria, hivyo kliniki hiyo ni fursa
muhimu kwa wananchi kupata msaada, ushauri na elimu ya sheria bila gharama.
Aidha, Mhe. Mghonto alisisitiza kuwa zoezi hilo ni
utekelezaji wa moja ya ahadi za Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya kuhakikisha kero
za wananchi zinatatuliwa kwa vitendo, huku akibainisha kuwa upatikanaji wa haki
ni msingi muhimu wa maendeleo ya jamii.
Kwa upande wake, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma
Homera,akizindua kliniki hiyo katika siku hiyo alisema kuwa lengo la kliniki ya
msaada wa kisheria ni kuwasaidia wananchi kupata haki zao kwa urahisi, pamoja
na kuwajengea uelewa kuhusu haki na wajibu wao kwa mujibu wa sheria za nchi.
Dkt. Homera aliongeza kuwa serikali itaendelea kusogeza
huduma za kisheria karibu zaidi na wananchi ili kuhakikisha kila Mtanzania
anapata haki bila vikwazo vya gharama au umbali.
Kliniki hiyo imepokelewa kwa furaha na wananchi wa Singida, wengi wao wakieleza kuwa huduma hiyo imekuwa msaada mkubwa katika kutatua migogoro ya ardhi, ndoa, mirathi na masuala mengine ya kisheria yanayowakabili katika maisha ya kila siku.







0 Comments