BAKWATA SINGIDA YAUNGA MKONO UJENZI WA UWANJA WA BOMBADIA KWA AJILI YA MEI MOSI KITAIFA 2025

 



Mkuu wa Mkoa akiongea na Shekh wa Mkoa Singida na kamati ya Mei Mosi taifa na Mkoa.




Waandisi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wakiangalia michoro mbalimbali ya ujenzi wa uwanja huo eneo la  jukwaa kuu.


Singida

Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Mkoa wa Singida limeungana na uongozi wa Mkoa huo katika jitihada za ujenzi wa Uwanja wa Bombadia, utakaotumika kwa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) Kitaifa yanayotarajiwa kufanyika mwezi ujao mjini Singida.

Sheikh wa BAKWATA Mkoa wa Singida, Sheikh Issa Nassor, ameongoza msafara wa walimu wa madrasa (Dini), wanafunzi wa madrasa, pamoja na Katibu wa JUWAKITA Mkoa Bi Khadija Ommari kwa upande wa wanawake , kwa ajili ya kushiriki kazi za ujenzi huo kwa vitendo kama ishara ya mshikamano na uzalendo.

Katika ziara yao katika eneo la ujenzi, Sheikh Nassor alipata fursa ya kukutana na Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, na kueleza namna vijana wa BAKWATA wanavyojitolea kushiriki katika maandalizi ya tukio hilo muhimu. Sheikh Nassor alisema kuwa ushiriki wa taasisi ya dini katika maendeleo ya kijamii ni sehemu ya jukumu la kiimani na kijamii kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mhe. Dendego aliipongeza BAKWATA kwa hatua hiyo ya kizalendo na kuwataka wadau wengine wa mkoa kuiga mfano huo, akisema kuwa maandalizi ya Mei Mosi ni suala la kila mwananchi wa Singida kwa kuwa mkoa unakuwa mwenyeji wa tukio la kitaifa litakalohusisha viongozi mbalimbali akiwemo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye atakuwa mgeni rasmi.

Naye Mhandisi Domisianus Kirina kutoka Sekretarieti ya Mkoa – Idara ya Miundombinu, amesema kuwa hadi sasa ujenzi wa uwanja huo umefikia asilimia 40, huku kazi ya ukamilishaji wa jukwaa kuu ikiwa inaendelea kwa kasi ili kuhakikisha eneo hilo linakuwa tayari kwa maadhimisho hayo muhimu.

Uwanja wa Bombadia unatarajiwa kuwa kitovu cha historia kwa Mkoa wa Singida, si tu kama mwenyeji wa Mei Mosi 2025, bali pia kama mfano wa ushirikiano wa kijamii kati ya taasisi za dini, serikali na wananchi kwa ujumla.

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments