RC DENDEGO AKABIDHI MAGARI MAPYA KWA WAKUU WA WILAYA SINGIDA

 










Singida –

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego, amekabidhi magari mapya kwa wakuu wa wilaya za Iramba, Ikungi, Manyoni pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Singida, ikiwa ni hatua ya kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Makabidhiano hayo yalifanyika katika viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida, ambapo Dendego aliwataka wakuu hao wa wilaya kuyatunza magari hayo ili yadumu na kusaidia katika utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

“Nawasihi myatumie magari haya kwa matumizi yaliyokusudiwa na myatunze ili yaweze kudumu kwa muda mrefu na kuwasaidia kutekeleza majukumu yenu kikamilifu,” alisema RC Dendego.

Awali, Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, akimkaribisha Mkuu wa Mkoa, alisema hadi sasa mkoa huo umepokea magari yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni mbili, yakiwemo magari ya huduma za afya na shughuli nyingine za utawala.

“Kupitia jitihada za Serikali, Mkoa wa Singida umepokea magari ya thamani ya zaidi ya shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kuboresha utoaji wa huduma mbalimbali, ikiwemo sekta ya afya,” alieleza Dkt. Mganga.

Makabidhiano hayo ni sehemu ya mpango wa Serikali wa kuimarisha miundombinu ya kiutendaji katika ngazi ya wilaya na kuhakikisha wananchi wanahudumiwa kwa ukaribu na kwa wakati.





Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments