RELI YA (SGR) NA BARABARA TOKA ITIGI MBEYA NI CHACHU YA UCHUMI -RC DENDEGO

 



Mkuu wa Mkoa Singida Halima Dendego akiongea na Kamati ya kudumu ya Bunge Miundombini katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Singida.


Wajumbe wa kamati ya kudumu ya Bumge ya miundombinu wakimsikilioza mkuu wa Mkoa wa Singida wakati akitoa Taarifa ya Mkoa huo katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.






Meneja wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini Mkoa wa Singida  Mhandisi Ibrahimu Kibasa akitoa Taarifa ya Tarura Mkoa wa Singida.


MKUU wa Mkoa wa Singida,Mhe.Halima Dendego amesema ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) pamoja na ujenzi wa barabara ya kutoka Itigi kwenda mkoani Mbeya utakapokamilika utachachua uchumi wa mkoa huo.

Amesema hayo jana (Mei 25, 2024) wakati akitoa maelezo kwa wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ambao walifanya ziara ya siku moja kukagua mradi wa ujenzi wa daraja la Minyughe na barabara ya lami katika Wilaya ya Ikungi.

Mhe.Dendego alisema mkoa upo katika mkakati wa kujenga bandari kavu ikiwa ni harakati za kukuza uchumi wa mkoa huu ambao pato la wananchi wake lipo chini ingawa jitihada kadhaa zinaendelea kuchukuliwa na serikali.

Naye Meneja wa Wakala wa Barabara wa Vijijini na Mijini (TARURA) Mkoa wa Singida,Mhandisi Ibrahimu Kibasa, alisema mkoa una mtandao wa barabara wenye kilomeya 5 669.412 ambapo za kiwango cha lami ni kilometa 51.11 sawa na asilimia 0.90 za changarawe ni kilometa 1,505.31 sawa na asilimia 26. 55 wakati za kiwango cha udongo zina urefu wa kilometa 4,112.992 sawa na asilimia 72.55.

Alisema katika  mwaka wa fedha wa 2023/2024 Mkoa wa Singida ulitengewa Sh.24,535,780,806.83 ambapo hadi kufikia Mei 20, 2024 zilikuwa zimepokelewa Sh.bilioni 13.281 sawa na asilimia 51.

Mhandisi Kibasa alisena TARURA ilifanya tathimini kukua barabara zilizoharibiwa na mvua ambazo zitaigharimu serikali Sh.bilioni 14.789 ambapo hadi sasa kiasi cha Sh.bilioni 1.628 zimepokelewa kwa ajili ya kuboresha barabara zilizoharibiwa na mvua na wakandarasi wameshaanza utekelezaji wa kazi katika maeneo mbalimbali.

Akizungumzia kuhusu daraja la Minyughe ambalo lilikatika na kusababisha kero kwa wakazi 28,339 wa kata za Maklawa na Minyughe ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 98 ambapo ilikuwa ibahusisha ukarabati wa daraja na matengenezo ya barabara kilometa 3 za maingilio ya daraja.

Mhandisi Kibasa alisema ujenzi wa daraja hilo ulikuwa unatekelezwa na mkandarasi JP Traders Limited kupitia fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Barabara kwa thamani ya Sh.milioni 556.140 na gharama za ununuzi wa vyuma ni Sh.bilioni 1.259,303,289 na hivyo kufanya jumla ya gharama kuwa Sh.bilioni 1.815.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Denis Londo aliitaka TARURA kwa kushirikiana na taasisi nyingine kuangalia uwezekano wa kuanza kuzalisha madaraja ya vyuma hapa nchini badala ya kuagiza nje ya nchi na kuigharimu serikali fedha nyingi.

"Ni wakati sasa wa kuangalia teknolojia ile ya madaraja ya vyuma tukaanza kuzalisha hapa nchini wenyewe kwa kutumia mahusiano yetu kati ya nchi na nchi badala ya kuendelea kuagiza nje tena kwa fedha za kigeni ambazo bado tuna changamoto nazo," alisema.

 Aidha, Londo aliitaka TARURA suala la ujenzi wa mifereje katika barabara zinazojengwa iwe agenda ya kudumu kwa nchi nzima vinginevyo serikali itakuwa inawekeza fedha katika ujenzi wa barabara ambazo hazitadumu kwa muda mrefu.

Naye Mtendaji Mkuu wa TARURA, Mhandisi Victor Seif alisema daraja la Minyughe wananchi kwa serikali wasaidie kulilinda lisiweze kuhujumiwa kwa kuibiwa vyuma na kwamba wakala ilishatoa maelekezo kwa mameneja wa mikoa na wilaya kila barabara zinapojengwa ziwe zinawekwa taa.

Alisema TARURA imeshafanya utafiti nchini nzima na kubaini kwamba kunahitajila taa 46,000 katika barabara zote zilizojengwa na pia wakala hivi sasa inaendesha kampeni ya kuelimisha wananchi utunzaji wa mitaro ya barabara ambayo imekuwa ikiharibika kutokana na watu kutupa taka ovyo na kusababisha izibe.

 

"Katika kuhakikisha mafanikio yanapatikana tumeinda kikosi maalum cha kutoa elimu ya kampeni hiyo ambacho kinafanya kazi kwa kushirikiana na wakurugenzi wa halmashauri ambapo kampeni imeanza katika mikoa ya Dodoma,Dar es Salaam na Mbeya," alisema.

Nao wabunge walisisitiza suala la kulilinda daraja hilo vyuma visiweze kuibiwa kwa kuweka taa kuanzia mwanzo hadi mwisho wa daraja na kwamba mitaro iwe inawekwa barabara zinapojengwa.

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments