SAKATA LA UTAKATISHAJI WA FEDHA LAMTIKISA AFISA ELIMU MKOA WA SINGIDA

 

 
Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Marshal Mseja,akingea na wanahabari mjini Singida.


    
      Watuhumiwa wakiwasili katika mahakama ya hakimu mkazi wa wilaya ya Singida


SINGIDA | 05 Juni 2025 –

 Afisa Elimu wa Mkoa wa Singida, Dkt. Elipidius Baganda, pamoja na wenzake wanne, wamefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Singida wakikabiliwa na tuhuma za utakatishaji wa zaidi ya shilingi milioni 44.

Kwa mujibu wa Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Marshal Mseja, aliyesoma hati ya mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Fadhil Luvinga, fedha hizo zilipaswa kutumika kwa shughuli za michezo ya shule za msingi kupitia mashindano ya UMITASHUMTA mwaka 2023. Hata hivyo, Dkt. Baganda anadaiwa kuzitumia kwa maslahi binafsi.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Evance Mlongo (mwalimu wa Shule ya Sekondari Mughanga), Paschal Kichambati (mkuu wa Shule ya Sekondari Mghanga), James Lazaro (Afisa Elimu Maalum, Manispaa ya Singida) na Deonatus Malima (Afisa Fedha, Manispaa ya Singida). Watatu wa mwisho wanashtakiwa kwa kutoa msaada katika kutekeleza kosa hilo.

Kwa sasa, Dkt. Baganda amenyimwa dhamana kutokana na uzito wa tuhuma dhidi yake na amepelekwa rumande. Mwalimu Evance Mlongo pia ameshindwa kutimiza masharti ya dhamana na amepelekwa rumande. Hata hivyo, washtakiwa wengine watatu wamefanikiwa kupata dhamana.

Kesi hiyo imepangwa kuendelea kusikilizwa tarehe 18 Juni 2025.

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments