SINGIDA
Jeshi la Zimamoto na
Uokoaji mkoa wa Singida limeendelea na jitihada zake za kutoa elimu kwa
wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi, likilenga kuhamasisha utunzaji wa
mazingira na kupunguza hatari ya majanga ya moto katika jamii.
Kaimu Kamanda wa Jeshi hilo, Mrakibu Debora Bigawa, amesema kuwa elimu hiyo inatolewa kama sehemu ya mikakati ya kuzuia majanga na kuhakikisha wananchi wanajua namna bora ya kutumia nishati salama majumbani mwao.
“Tunaendelea kuelimisha
jamii kuhusu matumizi ya nishati safi kama gesi na majiko bora, sambamba na
mbinu za kujikinga dhidi ya moto,” amesema Mrakibu Bigawa.
Aidha, amesema hadi
sasa hakujatokea matukio makubwa ya moto mkoani Singida, isipokuwa tukio moja
dogo lililoripotiwa hivi karibuni. Hata hivyo, amewataka wananchi kuendelea
kuwa waangalifu na kuchukua tahadhari mapema.
“Usalama ni jukumu la
kila mmoja wetu. Tunawashauri wananchi wahakikishe wana vifaa vya kuzimia moto
majumbani na mahali pa kazi, na wawe na uelewa wa hatua za kuchukua pale majanga
yanapotokea,” ameongeza.
Jeshi hilo limeeleza
kuwa litazidi kushirikiana na jamii kupitia kampeni na warsha mbalimbali ili
kuhakikisha elimu ya kinga dhidi ya moto inawafikia watu wengi zaidi, hasa
vijijini ambako uelewa bado ni mdogo.
Endelea
kufuatilia ukurasa wetu kwa taarifa zaidi kuhusu usalama wa moto na matumizi ya
nishati safi.
0 Comments