Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Mkalama Hajjat Asia Messos akitoa taarifa ya miradi mbalimbali ya maendeleo ya Halmshari ya Wilaya ya Mkalama kwa wanahabari.
Na Cales Katemana
Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama
imesema itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika mwaka wa
fedha 2026/27, ikilenga kuboresha huduma za elimu, afya pamoja na miundombinu
ya utawala kwa manufaa ya wananchi.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Mtendaji
wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, Hajjat
Asia Messos wakati akitoa taarifa
ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya wilaya kwa waandishi wa habari
wilayani Mkalama.
Hajjat Asia amesema katika sekta ya
elimu, halmashauri itajenga Shule mpya ya Sekondari Ishenga kupitia mradi wa
SEQUIP kwa gharama ya shilingi milioni 544, sambamba na kukamilisha maabara
katika shule za sekondari za Isanzu na Mwangeza, madarasa katika shule za
msingi za Ndala, Migunga na Mgolombyo, pamoja na ujenzi wa matundu ya vyoo
katika shule za Malaja, Ilunda na Kinandili.
Aidha, amesema kutakamilishwa nyumba
ya mwalimu katika Shule ya Msingi Kipamba, kujengwa bweni katika Shule ya
Sekondari Gunda, kutengenezwa vitanda 40 katika Shule ya Sekondari Mwangeza
pamoja na kununuliwa vifaa vya TEHAMA kwa Shule ya Sekondari Nduguti.
Katika sekta ya utawala, amesema
halmashauri itajenga nyumba tatu za wakuu wa idara kwa lengo la kuboresha
mazingira ya kazi, huku katika sekta ya afya ikikamilisha ujenzi wa Hospitali
ya Wilaya pamoja na vituo vya afya vya Ilunda na Gumanga.
Mkurugenzi huyo amesema pia
halmashauri itaendelea kuweka msisitizo katika kuwawezesha wananchi kiuchumi na
kuboresha huduma za elimu, afya, kilimo na mifugo ili kuongeza ustawi wa
wananchi na kuharakisha maendeleo ya wilaya.
Akizungumzia mafanikio ya mwaka wa
fedha 2025/26, Hajjat Asia ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa
na Rais kwa kuendelea kuipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama fedha za
kutekeleza miradi ya maendeleo, hatua ambayo amesema imechangia kuboresha utoaji
wa huduma kwa wananchi.
Pia amewapongeza watumishi wa
halmashauri, Mwenyekiti wa Halmashauri Mhe. Mohamed Juma, Baraza la Madiwani
pamoja na wananchi wa Mkalama kwa ushirikiano wao katika kusimamia na kutekeleza
miradi ya maendeleo.
Hajjat Asia amewataka wananchi
kuendelea kudumisha amani, kushirikiana na serikali kwa kutoa taarifa za
viashiria vya uhalifu au uvunjifu wa amani kwa viongozi wa vijiji na kata au
Ofisi ya Mkurugenzi.
Kwa upande wa watumishi wa umma,
amewahimiza kuongeza uwajibikaji, ubunifu na kasi ya utendaji kazi ili kutimiza
malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, akisisitiza kuwa maendeleo ya
Wilaya ya Mkalama yanategemea mshikamano na ushirikiano wa kila mmoja.




0 Comments