SINGIDA -IRAMBA
VIJANA wenye ulemavu mkoani Singida wametakiwa kujitokeza
kwa wingi kuchangamkia fursa mbalimbali za kiuchumi zinazotolewa na Serikali,
hususan mikopo ya asilimia 10 inayotengwa na halmashauri kwa ajili ya vijana,
wanawake na watu wenye ulemavu, ili kujiinua kiuchumi na kuboresha maisha yao.
Wito huo umetolewa na Afisa Maendeleo ya Vijana wa Mkoa wa
Singida, Frederick Ndahani, wakati wa ziara yake ya kukagua na kufuatilia
utekelezaji wa miradi ya vikundi vya vijana ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya
Iramba mkoani Singida.
Ndahani alisema Serikali imeweka mazingira rafiki pamoja na
sera jumuishi zinazolenga kuhakikisha watu wenye ulemavu hawabaki nyuma katika
mchakato wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Alisisitiza kuwa fursa hizo zipo
wazi kwa wote wanaokidhi vigezo na wenye dhamira ya dhati ya kufanya kazi.
“Serikali imedhamiria kuwawezesha vijana wote bila ubaguzi.
Vijana wenye ulemavu hawapaswi kuuona ulemavu wao kama kikwazo, bali kama
changamoto ya kugeuza fursa zilizopo kuwa chanzo cha maendeleo na ajira,”
alisema Ndahani.
Aliongeza kuwa mikopo hiyo inalenga kuwawezesha vijana
kuanzisha na kuendeleza shughuli za uzalishaji mali ikiwemo kilimo, ufugaji,
biashara ndogondogo na huduma mbalimbali, hatua itakayosaidia kupunguza utegemezi
na kuongeza kipato cha kaya.
Aidha, aliwasisitiza wanufaika wa mikopo hiyo kuitumia kwa
malengo yaliyokusudiwa, kusimamia miradi yao kwa uadilifu na kurejesha mikopo
kwa wakati ili kutoa nafasi kwa vijana wengine wengi zaidi kunufaika.
Ndahani aliwahakikishia vijana kuwa ofisi yake, kwa
kushirikiana na halmashauri, itaendelea kutoa ushauri, ufuatiliaji na mafunzo
ili kuhakikisha miradi yao inakuwa endelevu na yenye mafanikio ya muda mrefu.
Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Vijana wa Halmashauri ya
Wilaya ya Iramba, Peterson Ngahava, alisisitiza umuhimu wa nidhamu ya
urejeshaji wa mikopo kwa hiari na kwa wakati, akibainisha kuwa hatua hiyo
hujenga uaminifu kati ya vijana na Serikali na kuongeza wigo wa wanufaika wa
mikopo hiyo.
Baadhi ya vijana wenye ulemavu walionufaika na mikopo hiyo
wilayani Iramba waliishukuru Serikali kwa kuwawezesha, wakisema mikopo hiyo
imewapa matumaini mapya ya kujitegemea kiuchumi na kuwafanya wajione kuwa
sehemu muhimu ya jamii inayochangia maendeleo.
Walisema kupitia mikopo hiyo wamefanikiwa kuanzisha miradi
mbalimbali ya kiuchumi ambayo tayari imeanza kuwaletea kipato, huku wakiomba
kuendelea kupewa elimu ya ujasiriamali na usimamizi wa miradi ili kuongeza
tija.
Mmoja wa wanufaika hao, Abdallah Shalua, kijana mwenye
ulemavu wa ngozi, alisema alinufaika na mkopo wa Serikali wa shilingi milioni
saba (7,000,000) alioutumia kuanzisha na kuendeleza duka la bidhaa
mchanganyiko, jambo lililomwezesha kujitegemea kiuchumi na kuboresha maisha
yake.
Shalua aliwahimiza vijana wengine wenye ulemavu kutojisikia
kunyimwa fursa wala kukata tamaa, bali kutumia mikopo na programu mbalimbali za
Serikali kama chachu ya maendeleo yao binafsi na ya jamii kwa ujumla.
“Mkopo huu umebadilisha maisha yangu kwa kiasi kikubwa.
Umeongeza kipato changu na kunifanya niheshimike zaidi katika jamii. Serikali
imetuwekea mazingira rafiki ya kufanya kazi na kujitegemea, hivyo vijana wenye
ulemavu tusibweteke bali tushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi,”
alisema Shalua.
Katika ziara hiyo, Ndahani alitembelea Kikundi cha Vijana Blocks
kilichopo Kata ya Ndago kinachojishughulisha na ufundi wa ufyatuaji wa
matofali, pamoja na Kikundi cha Waoka Mikate cha Malisafi Bakery kilichopo
Shelui, ambavyo ni miongoni mwa vikundi vilivyonufaika na fursa za uwezeshaji
wa kiuchumi.
Ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kufuatilia utekelezaji wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa kwa vijana na makundi maalum, pamoja na kuhakikisha miradi inatekelezwa ipasavyo, inaendelea vizuri na kuleta tija kwa walengwa na jamii kwa ujumla.







0 Comments