Arusha
Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Februari 23, 2026
amezindua Shule ya Sekondari Sinya iliyopo Kata ya Sinya, Kijiji cha Leremeta,
Wilaya ya Longido mkoani Arusha, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali
kuendelea kuboresha miundombinu ya elimu nchini.
Shule hiyo
imejengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 1.2 zilizotokana na Serikali Kuu,
Mradi wa SEQUIP, TASAF pamoja na mapato ya ndani ya Halmashauri, huku wananchi
wakichangia shilingi milioni 34 kusaidia kukamilika kwa ujenzi wake.
Akizungumza
wakati wa uzinduzi huo, Dkt. Nchemba amesema uwekezaji huo unaonesha dhamira ya
Serikali ya kuhakikisha watoto wa Kitanzania wanapata mazingira bora ya
kujifunzia, sambamba na kupunguza changamoto ya umbali na msongamano wa wanafunzi
katika shule zilizopo.
Amesema
kukamilika kwa Shule ya Sekondari Sinya kutasaidia kuongeza nafasi za elimu ya
sekondari kwa wanafunzi wa Kata ya Sinya na maeneo jirani, na hivyo kuchochea
maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Wilaya ya Longido.
Aidha, Waziri
Mkuu amewahimiza wanafunzi kusoma kwa bidii ili kunufaika na fursa mbalimbali
zinazotolewa na Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,
ikiwemo programu ya ufadhili wa masomo ya Samia Scholarship.
Uzinduzi wa shule
hiyo ni kielelezo cha hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali katika
kuhakikisha elimu inabaki kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya Taifa.







0 Comments