SINGIDA YAADHIMISHA KUMBUKIZI YA KUZALIWA KWA BABA WA TAIFA KWA UPEKEE

 


Mgeni rasmi Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Mkoa wa Singiad Rajab Mussa akiongea na viongozi wa Taasisi hiyo ngazi ya Wilaya ya Singida vijijin


Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Wilaya ya Singida Vijijini akimkarubisha Mgeni Rasmi.


Naibu katibu Mkoa wa Singida wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Issa Slim akitoa maelezo mafupi.






Singida

Katika kuadhimisha kumbukizi ya siku ya kuzaliwa kwa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kongamano maalum limepangwa kufanyika tarehe 13 Aprili 2025 jijini Dodoma. Tukio hilo litahusisha mijadala ya kitaifa, maonyesho mbalimbali, na shughuli za kihistoria zitakazomulika mchango mkubwa wa Mwalimu Nyerere katika harakati za uhuru, ujenzi wa mshikamano wa kitaifa, na maendeleo ya Tanzania.

Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Mpango.

Kauli hiyo ilitolewa katika kikao cha kwanza cha uongozi mpya wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Wilaya ya Singida, kilichofanyika katika ukumbi wa Kituo cha Walimu Nyerere, mjini Singida.

Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Mkoa wa Singida, Rajab Shabani Musa, alitoa wito kwa viongozi wa ngazi zote kuiga na kuyaishi kwa vitendo maadili mema na misingi bora ya uongozi aliyoiacha Baba wa Taifa.

"Mwalimu Nyerere alikuwa kiongozi mwenye maono makubwa, mzalendo wa kweli na mpenda haki. Ni jukumu letu kama viongozi na wananchi kuyatunza maadili yake na kuyatumia kama dira ya maendeleo," alisema Rajab Musa.

Katika kudumisha maadili na historia hiyo kwa vizazi vijavyo, Mkoa wa Singida umeamua kuunda tume maalum chini ya mlezi wa taasisi hiyo mkoani, Mheshimiwa Halima Dendego. Tume hiyo itakuwa na jukumu la kutembelea, kutambua na kuhifadhi maeneo yote aliyowahi kufika Baba wa Taifa wakati wa uhai wake ndani ya Mkoa wa Singida.

Hatua hiyo inalenga kuyaweka maeneo hayo kama urithi wa taifa kwa ajili ya vizazi vijavyo, sambamba na kuimarisha kumbukumbu ya mchango wa Mwalimu Nyerere katika maendeleo ya Mkoa wa Singida na Tanzania kwa ujumla.

Aidha, taasisi hiyo imetoa wito kwa wananchi wote, hususan vijana, kushiriki kikamilifu katika shughuli mbalimbali za kumbukizi hizo, kwa lengo la kujifunza, kuhifadhi historia na kuendeleza mazuri yote aliyoyaacha Baba wa Taifa.

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments