KAMATI YA BUNGE YARIDHISHWA NA MIRADI YA TAWA MAKUYUNI

                              








Wajumbe wa kamati ya kudumu ya Bunge ilipotembelea eneo la Makuyuni na kujionea.

Na Happiness Shayo – Arusha

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imeridhishwa na utekelezaji wa miradi ya Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) ya ujenzi wa barabara (km 30) kwa gharama za shilingi milioni 256 pamoja na ujenzi wa bwawa kwa gharama ya shilingi milioni 125 katika Hifadhi ya Wanyamapori Makuyuni iliyopo Wilayani Monduli Mkoani Arusha ikiwa ni mojawapo ya maboresho katika kuendeleza uhifadhi, kukuza utalii na uwekezaji.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, Mhe.Timotheo Mnzava ameyasema hayo leo Machi 13,2025 wakati wa ziara ya kamati hiyo ya kukagua miradi hiyo Mkoani Arusha.

"Kipekee tuwapongeze TAWA wanafanya kazi nzuri hasa katika

kazi ya ukarabati na ufunguaji wa barabara na kazi ya utengenezaji wa bwawa" amesisitiza Mhe.Mnzava.

Aidha, Mhe. Mnzava ametoa wito kwa Menejimenti ya TAWA kuendelea kuitangaza hifadhi hiyo ili malengo yaliyokusudiwa, kutatua migogoro ya mipaka na kujenga mahusiano mazuri na jamii inayozunguka hifadhi hiyo.

Katika hatua nyingine Mhe. Mnzava amesema matamanio ya kamati hiyo ni kuiona TAWA inaendelea kubuni na kuwaza vyanzo vingine vya mapato ili iweze kujiendesha bila kutegemea fedha kutoka Serikali kuu.

Naye Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Balozi, Dkt.Pindi Chana (Mb) ameishukuru kamati hiyo  kwa maelekezo inayoyatoa mara kwa mara kwa Wizara yake ambapo amesisitiza kupitia maekezo hayo  Wizara ya Maliasili na Utalii imeweza kutekeleza na kuisimamia vizuri TAWA.

" Tunashukuru kwa maelekezo ya kamati lakini napenda kuielekeza TAWA hakikisheni hakuna migogoro ya mipaka na wakati umefika wa kulinda misitu yetu kwa sayansi na teknolojia mfano kwq kutumia kamera za kisasa, drones ili kuepusha uvamizi na ujangili" Mhe. Chana amesisitiza.

Pia, Mhe. Chana ametia mkazo suala la TAWA kujitangaza huku akiitaka Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kuhakikisha hifadhi hiyo inatangazwa ipasavyo ili kuvutia watalii.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii (anayeshughulikia Maliasili) CP Benedict Wakulyamba amesema kuwa Wizara inaendelea na mikakati mbalimbali ya kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu kwa kuchimba mabwawa, uongezaji wa vituo vya askari na kutumia teknolojia mbalimbali.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii iko Mkoani Arusha kwa ziara ya kikazi.

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments