WAZIRI MAVUNDE APIGA MARUFUKU WAGENI KWENYE LESENI ZA UCHIMBAJI MDOGO


 

Waziri wa Madini Antony Mavunde akiongea na wadau wa madini Mororogoro.


Rais wa Shirikisho la wachimbaji Madini Nchini Femata John Wambura Bina akiongea katika kikao kazi hicho.




Naibu katibu mkuu wa Wizara ya Madini Msafiri Mbibo akitoa ufafanuzi juu ya lengo la kikao hicho.
 


Na Mwandishi Wetu

Morogoro, Tanzania

Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amepiga marufuku wageni kuingia na kufanya shughuli za uchimbaji wa madini kwenye leseni za wachimbaji wadogo bila kufuata taratibu za kisheria. Hatua hii inakuja baada ya kugundulika changamoto katika mikataba ya utoaji wa msaada wa kiufundi kati ya wamiliki wa leseni ndogo za uchimbaji na wageni.

Mavunde alitoa tamko hilo leo, Februari 17, 2025, wakati wa kufungua Kikao Kazi cha wadau wa madini kilicholenga kupokea maoni juu ya rasimu ya Kanuni za Madini za Utoaji Msaada wa Kiufundi kwa Wamiliki wa Leseni Ndogo za Uchimbaji wa Madini. Mkutano huo umefanyika katika Ukumbi wa Edema Hoteli, Morogoro.

Akihimiza ushiriki wa wadau, Waziri Mavunde alisisitiza umuhimu wa kupata maoni ya wazi na yenye tija kwa ajili ya kuandaa kanuni bora zinazotekelezeka ili kuboresha sekta ya madini nchini. Pia alibainisha kuwa mabadiliko makubwa katika sekta hiyo yanatokana na utashi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye anahimiza maendeleo kwa wachimbaji wadogo.

"Haiwezekani mgeni aje, apate nafasi kupitia mkataba wa utoaji msaada wa kiufundi, lakini wachimbaji wadogo hawapati manufaa wala uboreshaji wa teknolojia na mitaji. Hili halikuwa lengo la sheria," alisema Mavunde.

Aidha, Waziri ametoa onyo kali kwa wachimbaji wadogo wanaowaruhusu wageni kuingia kinyemela kwenye leseni zao, akisema kuwa hatua kali, ikiwemo kufutiwa leseni, zitachukuliwa kwa watakaokiuka agizo hilo. Vilevile, amewaagiza Maafisa Madini wa Kanda (RMO) kuhakikisha wanadhibiti uingiaji wa wageni kwenye leseni ndogo bila kufuata taratibu husika.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo, amesema kikao hicho kinalenga kupata maoni ya wadau ili kuandaa rasimu ya kanuni hizo kwa uwazi na ushirikishwaji wa pande zote.

Naye Rais wa Shirikisho la Wachimbaji Wadogo wa Madini Tanzania, John Bina, amepongeza hatua ya serikali ya kuwashirikisha wadau katika uandaaji wa kanuni hizo, akisema kuwa ushirikishwaji huo utahakikisha kanuni zinazoandaliwa zinazingatia mahitaji halisi ya wachimbaji wadogo.

Mkutano huo umehudhuriwa na wadau mbalimbali wa sekta ya madini, wakiwemo viongozi wa wachimbaji wadogo kutoka mikoa yote nchini, vyama vya wachimbaji wadogo wanawake, na wafanyabiashara wa madini.

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments