TANZANIA NA CUBA KUSHIRIKIANA KATIKA UHIFADHI WA MALIASILI

    



Na Mwandishi wetu 

Serikali ya Tanzania na Jamhuri ya Cuba zimekubaliana kushirikiana katika sekta ya utalii na uhifadhi wa wanyamapori, hasa katika kukabiliana na changamoto ya mimea vamizi ndani ya maeneo yaliyohifadhiwa.

Makubaliano haya yamefikiwa , Februari 16 , 2025, katika kikao kilichofanyika jijini Dar es Salaam. Ujumbe wa Cuba umeongozwa na Balozi wa Tanzania nchini Cuba, Mhe. Humphrey Polepole, pamoja na Balozi wa Cuba nchini Tanzania, Mhe. Yordenis Despaigne Vera, huku upande wa Tanzania ukiwakilishwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Balozi, Dkt. Pindi Chana (Mb).

Waziri Dkt. Pindi Chana amewakaribisha nchini wataalamu saba kutoka Cuba kwa ajili ya kufanya utafiti wa kina kuhusu mimea vamizi inayozikumba hifadhi za taifa. Utafiti huu unalenga kutafuta suluhisho madhubuti katika kuimarisha uhifadhi wa maliasili.

"Mimea vamizi ni tishio kubwa kwa uhifadhi nchini, hasa katika Hifadhi ya Serengeti, Ngorongoro na Bonde la Ziwa Victoria. Spishi hizi zimevuruga mifumo ya ikolojia, kuathiri makazi ya wanyamapori, utalii, na maisha ya jamii za wenyeji," amesema Mhe. Chana.

Ameeleza kuwa mimea vamizi imeenea kutokana na shughuli za kibinadamu kama kilimo, biashara ya mimea ya mapambo, na juhudi za kudhibiti mmomonyoko wa ardhi. Kupitia ushirikiano huu, Tanzania itanufaika na teknolojia ya kisasa kutoka Cuba ili kukabiliana na changamoto hii na kuimarisha uhifadhi wa maliasili.

#Tanzania #Cuba #Uhifadhi #Utalii #MimeaVamizi #Serengeti #Ngorongoro

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments