MILIONI 75 ZAOKOLEWA SINGIDA: TAKUKURU YADHIBITI MATUMIZI YA FEDHA ZA MIRADI




Singida

Na Mwandishi Wetu 

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Singida imeokoa zaidi ya shilingi milioni 75 katika kipindi cha Oktoba hadi Desemba 2024 kupitia juhudi zake za kuzuia rushwa.

Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Singida Sipha Mwanjala, amesema kuwa zaidi ya shilingi milioni 65 ziliokolewa katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida na Wilaya ya Singida, hususan kwenye miradi ya ujenzi wa shule za sekondari Mwaja na Mtinko.

Katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, TAKUKURU iliokoa zaidi ya shilingi milioni 5, fedha ambazo zilikuwa ni makusanyo ya ushuru wa taka ngumu.

Kwa jumla, miradi 32 yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 13 ilifuatiliwa katika sekta za elimu, afya, mifugo, maji, na barabara mkoani Singida.

Katika programu ya TAKUKURU RAFIKI, taasisi hiyo imefanya vikao 10 na makundi mbalimbali ya wadau katika kata 10, ambapo jumla ya kero 24 ziliibuliwa na kushughulikiwa kupitia vikao 10 vya mrejesho

Kwa kipindi cha Januari hadi Machi mwaka huu, TAKUKURU Mkoa wa Singida imejiwekea mikakati ya kuendelea kufuatilia matumizi ya fedha za serikali katika miradi ya maendeleo, pamoja na kuendelea kutoa elimu kwa makundi mbalimbali kuhusu namna ya kuzuia vitendo vya rushwa.

Wananchi wanahimizwa kutoa taarifa za vitendo vya rushwa kwa kupiga simu ya bure namba 113, au kufika katika ofisi za TAKUKURU Mkoa wa Singida na wilaya za Iramba, Ikungi, Mkalama na Manyoni. 

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments