DC IRAMBA AGAWA HATIMILIKI ZA ARDHI NA KUKUZA MAENDELEO MBELEKESE

 


                            (picha kutoka maktaba yetu)


Na mwandishi wetu.

Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Dkt. Selemani Mwenda, amegawa hatimiliki za kimila 500 na hati za viwanja 5,000 kwa wakazi wa Kata ya Mbelekese ili kuimarisha umiliki halali wa ardhi na kuzuia migogoro ya ardhi.

Hatimiliki hizo zimetolewa kwa vijiji vya Usure, Mbelekese, na Kikonge, zikiwa na lengo la kuondoa migogoro ya kifamilia hasa wakati wa mirathi au talaka.

Diwani wa Kata ya Mbelekese, Omari Shabani Wawa, amemshukuru DC Mwenda kwa juhudi hizo na kusisitiza kuwa hatua hiyo itasaidia sana jamii. Pia, mashirika yasiyo ya kiserikali—Adventus na Ukijani—yamechangia miti na mbegu kwa ajili ya mazingira na kutoa mizinga 60 yenye thamani ya Sh 9 milioni kwa ajili ya ufugaji wa nyuki.

Zaidi ya kilo 800 za majani kwa lishe ya mifugo zilitolewa kwa wafugaji, huku wakulima 20 wakipimwa udongo wa mashamba yao ili kuboresha mazao. Wananchi walijitokeza kwa wingi kupima afya, ambapo chupa 15 za damu zilichangwa, watu 74 walipimwa afya, na 100 walipimwa presha na uzito.

Katika sherehe hizo, vikundi vya akinamama vilileta miche 1,000 ya miti kwa ajili ya biashara, huku wakazi wa Mbelekese wakihamasishwa kuanzisha ufugaji wa samaki. Wakulima pia wamehamasishwa kutumia mbolea na mbegu bora ili kuongeza uzalishaji, huku viwanda vidogo vinne vya mafuta ya alizeti vikichochea kilimo cha zao hilo.

Wananchi wamempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha huduma za kijamii na maendeleo ya kiuchumi, wakiahidi kumuunga mkono katika uchaguzi ujao.

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments