Kamishina Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida Shamimm Hoza akiongea baada ya ufunguzi wa mafunzo hayo yaliyofanyika mkoani Singida.
SINGIDA
Mfumo wa kidijitali wa e-Ardhi unatarajiwa
kuleta mageuzi makubwa katika utoaji wa huduma za ardhi kwa wananchi wa Mkoa wa
Singida, kwa kupunguza misongamano, mizunguko isiyo ya lazima pamoja na muda wa
kufuatilia huduma katika ofisi za ardhi.
Kupitia mfumo
huo, wananchi wataweza kupata huduma mbalimbali za ardhi kwa njia ya mtandao,
hatua inayolenga kuongeza ufanisi, uwazi na urahisi wa upatikanaji wa huduma.
Akizungumza
Septemba 14, 2026, mkoani Singida wakati wa mafunzo kuhusu uendeshaji wa mfumo
huo na namna wananchi watakavyonufaika nao, Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa
Singida, Bi. Shamim Hoza, amesema e-Ardhi itasaidia kuboresha kwa kiasi kikubwa
utoaji wa huduma za ardhi.
Bi. Hoza amesema
mfumo huo utapunguza msongamano wa wananchi katika ofisi za ardhi, kuondoa
mizunguko isiyo ya lazima katika kufuatilia huduma na kuongeza uwazi katika
utoaji wa huduma.
“Mfumo huu
utaongeza uwazi na kupunguza msongamano usio wa lazima katika ofisi zetu,”
amesema Bi. Hoza.
Aidha, Kamishna
Hoza amewataka wataalamu wa ardhi katika Mkoa wa Singida kuupokea mfumo huo na
kuhakikisha wanakuwa na uelewa na uwezo wa kuutumia ipasavyo, akieleza kuwa ni
hatua muhimu kuelekea utoaji wa huduma bora zaidi kwa wananchi.
Kwa upande wake,
Afisa Ardhi wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida, Ibrahim Magessa, amesema mfumo
huo utarahisisha upatikanaji wa huduma za ardhi kwa wananchi, hususan katika
kuomba nyaraka mbalimbali ikiwemo hati za umiliki wa ardhi.
Naye Afisa
Mipango Miji wa Manispaa ya Singida, Koletha Timanywa, amesema mafunzo hayo ni
muhimu kwa wataalamu wa ardhi kutokana na kasi ya maendeleo ya sayansi na
teknolojia.
Amesema ni jukumu
la wataalamu hao kuhakikisha wanaufahamu na kuumudu mfumo wa e-Ardhi ili
kuongeza ufanisi na kuboresha zaidi huduma wanazowapatia wananchi.





0 Comments