UONGOZI WA TUGHE WAIPONGEZA MAHAKAMA KANDA YA DODOMA







Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) wameipongeza Mahakama Kanda ya Dodoma kwa kuwajali watumishi ikiwa ni pamoja na kuzingatia maslahi yao.

Pongezi hizo zilitolewa na Viongozi hao waliohudhuria katika kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kanda ya Dodoma kilichofanyika jana tarehe 24 Aprili, 2024 mkoani Singida. 

Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa TUGHE Mkoa wa Singida, Dkt. Athuman Bunto alisema, “naipongeza sana Mahakama kwa kuzingatia na kufuata Sheria za utumishi kwani wamezingatia maslahi ya watumishi, sehemu kubwa ya bajeti inawagusa watumishi, mafunzo kutolewa katika Kada zote kwa ajili ya kujengeana uwezo, hiki ni kitu kizuri.”

Aidha, amelisifu Baraza hilo kuwa, limeendeshwa kwa uwazi watumishi wameonekana kuridhika na limekuwa shirikishi kwani hoja zilizotolewa zilipatiwa majibu na kwa zile ambazo zilikuwa chini ya uwezo wa Kanda wajumbe wamekubaliana kuziwasilisha katika Baraza Kuu.

Kikao hicho kiliongozwa na Mhe Jaji Mfawidhi  Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt Juliana Masabo ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza hilo.

Katika Baraza hilo, taarifa za bajeti zilisomwa kutoka Mikoa yote Miwili ya Singida na Dodoma na kuona utekelezaji wake hususani kwenye maeneo yanayowahusu watumishi moja kwa moja na pia kuona vipaumbele vya bajeti kwa mwaka wa fedha 2024/2025.

Akihitimisha kikao cha Baraza hilo, Mhe. Dkt. Masabo aliwasisitiza watumishi kuendelea kuwaelekeza na kuwasaidia wateja wanaofika mahakamani kuhusiana na mabadiliko ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano TEHAMA na Mifumo mbalimbali ya Mahakama kwa kuwatia moyo na kuona mabadiliko ya TEHAMA ni msaada kwao.

Vilevile, aliwataka wajumbe wa Baraza kuzingatia azimio la Morogoro kuhusu utunzaji wa Mazingira kwa kuendelea kutunza mazingira na kupanda miti ya vivuli na matunda.



Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments