SINGIDA
Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetoa kibali kwa
Shirika la Mtandao wa Mashirika ya Wasaidizi wa Kisheria Nchini (TANLAP) kutoa
elimu ya mpiga kura katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwa ni sehemu ya juhudi
za kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu taratibu za kupiga kura kuelekea uchaguzi
mkuu utakaofanyika Oktoba 29, mwaka huu.
Msaidizi wa kisheria kutoka TANLAP mkoani Singida, Theresia
Mande, akizungumza na wananchi katika Soko Kuu la Kimataifa la Vitunguu
Singida, amewahimiza wananchi kuzingatia taratibu zote zilizowekwa na NEC,
ikiwemo kuhakikisha kila mtu anapiga kura katika kituo alichojiandikishia.
Aidha, Mande amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi na kwa
wakati siku ya uchaguzi ili kutumia haki yao ya kikatiba ya kupiga kura.
“Kwa mwaka huu, Tume imeweka utaratibu utakaowawezesha
wafungwa kushiriki kupiga kura ya urais pekee, ambapo vituo vya magereza
vitafunguliwa saa 2:00 asubuhi na kufungwa saa 9:00 alasiri, huku vituo vingine
vilivyopo uraiani vitafunguliwa saa 1:00 asubuhi hadi saa 10:00 jioni,” amesema
Mande.
Ameongeza kuwa kupiga kura ni haki ya msingi ya kila raia
mwenye umri wa kuanzia miaka 18 na kuendelea, huku akisisitiza umuhimu wa kutoa
kipaumbele kwa wazee, kina mama wajawazito, wenye watoto wachanga, pamoja na
watu wenye ulemavu watakaofika vituoni.
Elimu hiyo imeendelea kutolewa katika maeneo yenye mikusanyiko ya watu kama masokoni, vituo vya mabasi na maeneo ya wazi, lengo likiwa ni kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kuhusu utaratibu wa uchaguzi na kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kidemokrasia.






0 Comments