WANANCHI WATAKIWA KUILINDA MIUNDOMBINU YA SHULE MPYA SINGIDA

 



Na Mwandishi Wetu – Singida

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ametoa wito kwa wananchi wote wa mkoa huo kushirikiana na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kulinda na kutunza miundombinu ya shule mpya zilizojengwa kwa lengo la kuinua kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi.

Akizungumza wakati wa kufanya tathmini ya hali ya elimu mkoani Singida, Mhe. Dendego alisema kuwa juhudi kubwa zimefanyika katika sekta ya elimu, ikiwemo ujenzi wa shule mpya, ili kutoa fursa kwa wanafunzi kusoma katika mazingira bora na rafiki kwa ujifunzaji.

“Mkoa wetu umejipanga kuimarisha sekta ya elimu kupitia maboresho makubwa yanayofanywa na Serikali. Tunahitaji ushirikiano wa wananchi kuhakikisha miundombinu hii inadumu na kuwanufaisha vizazi vya sasa na vijavyo,” alisema Dendego.

Kwa mujibu wa Mhe. Dendego, jumla ya shule 30 za kata zimejengwa kupitia Mradi wa Kuimarisha Ubora wa Elimu ya Sekondari (SEQUIP). Aidha, shule mpya ya wasichana ya Solya imejengwa katika Wilaya ya Manyoni, huku shule mbili za amali – Kitukutu (Iramba) na Unyambwa (Singida Manispaa) – zikikamilika na kuanza kutoa huduma kwa wanafunzi.

Amesisitiza kuwa wananchi wanapaswa kuwa walinzi wa miundombinu hiyo kwa kuhakikisha inatunzwa ipasavyo na kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa ili kuinua ubora wa elimu kwa ujumla.

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments