SINGIDA
Mbunge wa
Jimbo la Singida Mjini, Mhe. Yagi Kiaratu, amezungumza na wazee wa Manispaa ya
Singida katika mkutano maalum uliofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Ufundi
Stadi (VETA) mjini Singida.
Mkutano huo ulifunguliwa rasmi na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi
(CCM) Wilaya ya Singida, Bi. Lucia Mwiru, na kuhudhuriwa na wazee maarufu
kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa huo, viongozi wa dini, wastaafu waliowahi
kushika nyadhifa tofauti za uongozi katika mkoa wa Singida, pamoja na wataalamu
kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Singida.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Yagi Kiaratu alipata fursa ya
kusikiliza kero na changamoto mbalimbali zilizowasilishwa na wazee hao, ambapo
alijibu maswali yao papo kwa papo na kutoa ufafanuzi juu ya masuala yanayohusu
maendeleo ya jimbo hilo. Aidha, alipokea salamu za Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania zilizotolewa na wazee mbalimbali waliohudhuria mkutano huo.
Mbunge huyo aliwataka wazee kuendelea kuwa nguzo ya amani kwa
kushirikiana kwa karibu na vijana wao, ili kuepusha uvunjifu wa amani
ulioshuhudiwa hivi karibuni katika baadhi ya kata na mikoa nchini. Alisisitiza
kuwa wazee wana nafasi kubwa katika kutoa malezi, ushauri na maelekezo sahihi
kwa vijana ili kudumisha mshikamano na utulivu wa jamii.
Pia, Mhe. Yagi Kiaratu alitumia fursa hiyo kuwashukuru wananchi wa
Singida Mjini, hususan wazee, kwa kumuamini na kumchagua kuwa Mbunge wa jimbo
hilo katika Uchaguzi Mkuu uliopita, akiahidi kuendelea kushirikiana nao katika
kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya Singida.
Mkutano huo
ulimalizika kwa wazee kupongeza hatua ya Mbunge wao kukutana nao ana kwa ana na
kusikiliza maoni yao, wakieleza matumaini makubwa ya kuendelea kushirikiana na
uongozi wa serikali kwa maendeleo na ustawi wa jamii ya Singida.






0 Comments