Waziri Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba akiongea na watumishi baada ya kukagua mradi huo.
PWANI
Na Mwandishi wetu
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu
Nchemba, leo Desemba 29, 2025, amefanya ziara ya ukaguzi katika eneo la Ruvu
Chini, mkoani Pwani, kukagua hali ya uzalishaji na usambazaji wa maji.
Ziara hiyo imelenga kujionea kwa karibu utekelezaji wa
miradi ya maji pamoja na hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kukabiliana
na changamoto ya upungufu wa maji inayochangiwa na mabadiliko ya tabia ya nchi.
Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Dkt. Mwigulu amesema kuwa
Serikali ilianza mapema kutambua changamoto ya upatikanaji wa maji na hivyo
kuanza kutekeleza miradi mikubwa ya maji katika kipindi cha miaka mitatu
iliyopita.
Amesisitiza kuwa mipango hiyo haikuanza kwa bahati mbaya,
bali ilitokana na tathmini ya kina iliyofanywa na Serikali kuhusu athari za
mabadiliko ya tabia ya nchi, ambapo juhudi kubwa zimeelekezwa katika ujenzi wa
miradi ya kimkakati inayolenga kutoa suluhisho la kudumu kwa wananchi.
“Mipango hii ya ujenzi wa miradi ya maji ilianza muda mrefu.
Serikali iliona changamoto mapema na kuanza kutafuta majawabu yake miaka mitatu
iliyopita kwa kujenga miradi mikubwa itakayotoa matokeo chanya kwa wananchi,”
amesema Dkt. Mwigulu.
Serikali imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuhakikisha
wananchi wanapata maji safi na salama kwa uhakika, huku miradi kama ya Ruvu
Chini ikitarajiwa kuongeza upatikanaji wa maji kwa maeneo ya Pwani na Dar es
Salaam kwa ujumla.








0 Comments