WAZIRI MKUU DKT MWIGULU AAMURU HATUA KALI KWA MKANDARASI ALIYEKWAMA KUKAMILISHA BANDARI KAVU MANYONI

 

Waziri Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba ameanza ziara Mkoani Singida akiwa Manyoni amekagua Mradi wa Bandari Kavu na Kutoa maelekezo juu ya Mkandarasi.



Na Cales Katemana

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, ameanza rasmi ziara yake ya pili mkoani Singida, ikiwa ni mwendelezo wa ukaguzi wa miradi ya kimkakati inayotekelezwa katika mkoa huo. Ziara hii inafuatia ukaguzi alioufanya katika Hospitali ya Mkoa wa Singida hivi karibuni.

Katika siku ya pili ya ziara hiyo, Dkt. Nchemba ametembelea kwa mara ya kwanza mradi wa ujenzi wa Bandari Kavu (Dry Port) wilayani Manyoni, mradi ambao umekuwa ukisuasua kwa muda mrefu.

Akiwa eneo la mradi, Waziri Mkuu alielezwa kuwa ujenzi wa bandari hiyo umesimama kwa zaidi ya miaka nane, baada ya mkandarasi kushindwa kukamilisha mradi na kudaiwa kufilisika.

Mradi huo, unaojulikana kama Construction of One Stop Inspection Station (OSIS) – Lot 1, ulianza kutekelezwa Mei 2017 na ulipaswa kukamilika Novemba 2018. Mkandarasi aliyekuwa amepewa jukumu la ujenzi ni Impress di Construczioni Ing. E, ambapo thamani ya mradi inakadiriwa kufikia Euro 9,537,607.90, sawa na Shilingi za Tanzania 26,823,568,457.96.

Katika kuhakikisha nidhamu na uwajibikaji unazingatiwa, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu ameagiza mamlaka husika kukamata pasipoti ya mkandarasi huyo, hadi pale atakapokamilisha mradi au kuukabidhi rasmi kwa serikali ili hatua nyingine ziendelee.

Aidha, amesisitiza kuwa serikali haitavumilia miradi ya maendeleo kusimama kwa muda mrefu, hasa ikizingatiwa umuhimu wake kwa wananchi na uchumi wa taifa.

“Hatutaacha miradi kukaa miaka mingi bila kukamilika wakati wananchi wanahitaji huduma. Lazima thamani ya fedha ionekane,” amesisitiza Dkt. Mwigulu.

Wakazi wa Manyoni na Mkoa wa Singida kwa ujumla wamesema wana matumaini makubwa kuwa hatua zilizochukuliwa na serikali zitafungua njia ya kukamilika kwa mradi huu muhimu, ambao ukikamilika utarahisisha shughuli za usafirishaji, ukaguzi na biashara katika ukanda wa kati.

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments