FEMATA YAPITISHA MAAZIMIO SABA MUHIMU KATIKA KIKAO CHAKE CHA KWANZA BAADA YA UCHAGUZI.

Rais wa Shirikisho la wachimbaji madini wadogo nchini FEMATA akiongea katika kikao cha Sekretariet .

 





                             

                  Kamisha wa madini Terence Ngole akiongea na wajumbe wa sekretariet katika kikao maalum kilochofanyika jijini Dodoma.       

                           

DODOMA

Shirikisho la Wachimbaji Wadogo wa Madini Nchini (FEMATA) limefanya kikao chake cha kwanza cha sekretarieti baada ya Uchaguzi Mkuu wa Awamu ya Sita, kikao kilichofanyika jijini Dodoma katika ukumbi wa African Dreams Hotel.

Kikao hicho kimeongozwa na Rais wa FEMATA, John Bina, sambamba na Makamu Rais Victor Tesha, na Katibu Mkuu Elies Rodgers. Washiriki walikuwa ni wajumbe wa kamati mbalimbali za shirikisho hilo pamoja na viongozi wa wachimbaji wadogo kutoka mikoa yote nchini.

Mgeni rasmi alikuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahaya Samamba, aliyewakilishwa na Kaimu Kamishna wa Madini, Terence Ngole.

Katika kikao hicho, FEMATA imeipongeza Serikali kupitia Wizara ya Madini chini ya uongozi wa Waziri Anthony Mavunde na Naibu Waziri wake, kwa jitihada mbalimbali za kuboresha sekta ya madini na kuweka mazingira rafiki kwa wachimbaji wadogo.

Sekretarieti imejadili kwa kina mustakabali wa sekta ya uchimbaji mdogo na kupitisha maazimio saba ,Femata itayakabidhi maazimio hayo kwa Waziri wa Madini mwezi Januari.

1-Kuondoa migongano ya kimasilahi katika shughuli za uchimbaji na kuboresha mifumo ya utatuzi wa migogoro.

2-Kuandaa mpango kazi wa FEMATA utakaowasilishwa rasmi serikalini kwa utekelezaji.

3-Kuthibitisha msimamo kuwa FEMATA si chama cha kiarakati, bali ni chombo cha majadiliano na ushirikiano wa kiserikali.

4-Kuimarisha mahusiano kati ya wachimbaji wadogo na makamishna wa madini katika mikoa.

5-Kuunda na kuimarisha Kamati ya Maadili itayosimamia nidhamu na matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii.

6-Kuomba serikali iendelee kuwajengea uwezo wachimbaji wadogo ili kuongeza tija na usalama migodini.

7-Kutafuta ufumbuzi wa changamoto ya nishati migodini, ikiwemo upatikanaji wa umeme na mafuta kwa gharama nafuu.

FEMATA pia imeomba serikali kuharakisha mpango wa kuitangaza Tanzania kama kitovu cha biashara ya madini Afrika, kwa kuweka mazingira bora zaidi kwa wauzaji, wanunuzi na wawekezaji.

Kwa mujibu wa takwimu, zaidi ya asilimia 70 ya vijana nchini wanajihusisha na shughuli za uchimbaji madini, huku FEMATA ikiwa na wanachama wanaokadiriwa kufikia milioni 6.





Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments