HALIMA DENDEGO AWATAKA VIONGOZI WA BAKWATA KUWA MFANO WA MAADILI MEMA.

Dc Gondwe akifunga Mkutano Mkuu wa Bakwata Mkoa wa Singida kwaniaba ya Mkuu wa Mkoa wa Singida Halima Dendego.

Katibu wa Bakwata Mkoa wa Singida Ustadh Ommary Muna akiongea katika uchaguzi huo.

                                  
                                      


                              
                              
                   

             
                     



SINGIDA

Na Cales katemana

Viongozi wateule wa Baraza la Waislam (BAKWATA) Mkoa wa Singida wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maadili ya katiba na kanuni za baraza hilo, ili kuimarisha umoja, nidhamu na uadilifu katika uongozi wa dini.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, wakati akihitimisha uchaguzi wa viongozi wa BAKWATA ngazi ya mkoa, uliofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, amesema kuwa BAKWATA ni taasisi muhimu inayopaswa kuwa kioo cha waumini wa dini ya Kiislam, hivyo viongozi wapya wanapaswa kufanya kazi kwa bidii, uadilifu, na kuzingatia malengo ya baraza hilo.

“BAKWATA ni kioo cha jamii ya Kiislam, hivyo viongozi mnapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika utendaji, mshikamano na maadili,” alisema Gondwe.

Aidha, Mhe. Gondwe amewahakikishia viongozi wapya kuwa Serikali ya Mkoa wa Singida chini ya uongozi wa Mkuu wa Mkoa Mhe. Halima Dendego, itaendelea kushirikiana nao sambamba na taasisi zote za kidini bila ubaguzi wa imani.

Katika hatua nyingine, akizungumzia suala la amani ya nchi, Mhe. Gondwe amewataka viongozi wa dini kushiriki kikamilifu katika kuhamasisha amani, hususan katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29 mwaka huu.

“Ni muhimu viongozi wa dini kuwa mstari wa mbele katika kudumisha amani na kuhamasisha waumini kujitokeza kupiga kura kwa amani na utulivu,” alisisitiza.

Uchaguzi huo wa BAKWATA Mkoa wa Singida ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa dini na serikali, na ulilenga kuweka safu mpya ya uongozi itakayotekeleza majukumu kwa mujibu wa katiba ya baraza hilo.





Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments