
SINGIDA
Na Cales Katemana
Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima
Dendego, amewataka vijana wenye vipaji mbalimbali mkoani humo kujitokeza kwa
wingi kuonesha vipaji vyao ili serikali iweze kuvibaini na kuvikuza kupitia
wataalamu waliopo.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa
tamasha kubwa la "Singida Pamoja Dancing" lililofanyika katika
viwanja vya Bombadia mjini Singida, Mhe. Dendego alisema kuwa sanaa kwa sasa ni
ajira yenye kipato kinachoweza kubadilisha maisha ya vijana wengi.
Alitolea mfano nyota wa kimataifa
waliotokea Singida akiwemo mwanariadha Felix Simbu na mchezaji wa timu ya taifa
ya wanawake, Twiga Stars, anayekipiga soka la kulipwa Aisha Msaka, akisema kuwa
ni mifano halisi ya namna vipaji vinavyoweza kumuinua kijana na taifa kwa
ujumla.
Akijibu risala ya washiriki na
waandaaji wa tamasha hilo, Mkuu wa Mkoa alisema ameyapokea maombi yao na
atayafanyia kazi mara moja. Pia aliwataka vijana kutojihusisha na vitendo vya
uvunjifu wa amani, badala yake wawe wabunifu na wachapa kazi kwa maendeleo yao
na ya mkoa mzima.
Aidha, aliwahimiza vijana kujitokeza
kwa wingi kushiriki katika uchaguzi utakaofanyika Oktoba 29, akisema ni fursa
muhimu ya kuchagua viongozi watakaowawakilisha vyema.
Tamasha hilo lilihusisha vijana kutoka
vyuo mbalimbali, shule za msingi na sekondari kutoka maeneo tofauti ya mkoa wa
Singida. Pia lilipambwa na burudani mbalimbali zikiwemo michezo ya dansi, nyama
choma, na mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Yanga na Silver Strikers ya
Malawi, iliyotazamwa mubashara na mashabiki wa soka waliofurika uwanjani.






0 Comments