ASP KAYOMBO: WATUMISHI WAASWA KUFUATILIA MALEZI YA WATOTO KWA UKARIBU

 



Na Eric Amani – Dodoma

Watumishi wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wametakiwa kuwa karibu zaidi na watoto wao kwa kufuatilia kwa ukaribu mwenendo na malezi yao ili kujenga jamii yenye maadili bora.

Wito huo umetolewa leo, Jumatatu Julai 21, 2025 na Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Dodoma, Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Christer Kayombo, wakati wa muendelezo wa mafunzo ya kila wiki kwa watumishi wa ofisi hiyo.

ASP Kayombo amesema visa vingi vya ukatili dhidi ya watoto vimekuwa vikichochewa na wazazi au walezi kushindwa kuwajibika ipasavyo katika malezi ya watoto wao.

“Wazazi wengi wamekuwa wakiwatelekeza watoto wao mikononi mwa wafanyakazi wa majumbani na hivyo kutoa mianya ya vitendo vya ukatili na uhalifu kufanyika,” alisema ASP Kayombo na kuongeza:

“Tengeni muda wa kuwafuatilia watoto wenu pindi mnapotoka kazini. Msiachie jukumu hilo kwa wengine. Simameni kama walezi wa kweli na wenye kuwajali watoto.”

Aidha, aliwataka watumishi hao kuwa mfano wa kuigwa katika jamii kwa kulea watoto wao katika misingi ya maadili mema na kuimarisha mahusiano ya kifamilia.

Katika hatua nyingine, ASP Kayombo aliwahimiza kuwa mabalozi wa kupinga vitendo vya ukatili—majumbani, maofisini na katika jamii kwa ujumla.

“Ni matumaini yangu kuwa baada ya mafunzo haya, matendo ya ukatili dhidi ya watoto na vitendo visivyofaa vitapungua katika jamii,” alihitimisha ASP Kayombo.

Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments