Khadija Abdala wa Mtaa wa Mji wa zamani wa kwanza juu na Johari Juma wa Mtaa wa Nghongoajibu wa pili wakazi wa manispaa ya Singida wakilalamika kukosa maji.
Meneja wa Suwasa Singida Sebastian Warioba ametoa ufafanuzi kupita Meneja uzalishaji maji na usambazaji Mamlaka ya Maji Singida.
SINGIDA
Baadhi ya wakazi wa Kata ya Mughanga na Mitaa ya Ghongwajibu, iliyopo katika Kata ya Kindai, Manispaa ya Singida, wameiomba Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Singida (SUWASA) kufafanua sababu za kutokuwepo kwa huduma ya maji kwa muda mrefu katika maeneo yao, hali ambayo imesababisha usumbufu mkubwa kwa jamii bila taarifa yoyote rasmi kutoka kwa mamlaka hiyo.
Wakizungumza katika semina ya siku moja iliyoandaliwa na Mamlaka ya
Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji Kanda ya Kati (EWURA), wakazi hao
walieleza kuwa wamekuwa wakikosa huduma hiyo ya msingi kwa kipindi kirefu na
kuona kimya cha mamlaka hiyo kama kutowajali walaji.
“Hali ni ngumu, maji hayapatikani kabisa na hakuna hata taarifa.
Hatujui tuamini nini,” alisikika mkazi mmoja akilalamika mbele ya wawakilishi
wa EWURA.
SUWASA Yatolea Ufafanuzi
Kufuatia malalamiko hayo, blogu hii ilifika katika ofisi za SUWASA
mjini Singida kufuatilia suala hilo. Meneja wa Uzalishaji Maji na Usambazaji
kutoka SUWASA, Mhandisi Elisha Kivuyo, alitoa ufafanuzi kuhusu chanzo cha
changamoto hiyo.
Kulingana na Mhandisi Kivuyo, tatizo hilo lilisababishwa na
kuharibika kwa mota ya kusukuma maji katika kisima cha LITI kilichopo Kata ya
Ipembe, jambo lililoathiri upatikanaji wa huduma ya maji katika baadhi ya
maeneo ya Kata za Ipembe na Kindai, ikiwa ni pamoja na vitongoji kadhaa
vilivyopo pembezoni.
“Hili ni tatizo la kiufundi lililotokea ghafla. Mota ya kusukuma
maji iliharibika, jambo lililosababisha usumbufu mkubwa. Hata hivyo, tunapenda
kuwataarifu wananchi kuwa mota hiyo tayari imetengenezwa na huduma ya maji
imeanza kurejea kwa awamu,” alisema Mhandisi Kivuyo.
Aliongeza kuwa licha ya changamoto hiyo ya kifundi, SUWASA
inaendelea kuchukua hatua za kudumu za kuboresha miundombinu ya maji ili
kuhakikisha huduma inapatikana kwa uhakika na kwa wakati kwa wakazi wa Manispaa
ya Singida.
“Tunaelewa umuhimu wa maji kwa wananchi, na ndio maana tunafanya
kazi usiku na mchana kurejesha huduma hiyo. Tunaomba radhi kwa usumbufu
uliojitokeza,” aliongeza Kivuyo.
0 Comments