EWURA YATOA MAFUNZO YA MATUMIZI SALAMA YA GESI KWA WAKAZI WA SINGIDA

 


Mkurugenzi wa kanda ya kati Mamlaka ya Udhibiti wa huduma za nishati na Maji EWURA kanda ya Kati Hawa Luweno akitoa ufafanuzi katika semina hiyo.






Wataalamu mbalimbali kutoka EWURA kanda ya kati na Jeshi la Zimamoto mkoa wa Singida wakitoa Elimu juu ya kujikinga na majanga ya Moto.



                             


SINGIDA DIGITAL

Wakazi wa Mkoa wa Singida waliokusanyika kwa ajili ya semina ya siku moja kuhusu matumizi salama ya gesi ya kupikia wameipongeza Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), kwa hatua yake ya kuwakutanisha wadau na kutoa elimu muhimu kuhusu usalama wa matumizi ya nishati hiyo.

Semina hiyo ilifanyika katika ukumbi wa RC Mission mjini Singida na kuhudhuriwa na wauzaji na watumiaji wa gesi kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa huo. Lengo kuu la semina ilikuwa ni kutoa mwanga juu ya matumizi bora ya gesi, namna ya kuhifadhi mitungi kwa usalama, na hatua za tahadhari ili kuepuka ajali zinazotokana na uzembe au uelewa mdogo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya washiriki waliishukuru EWURA kwa kuandaa semina hiyo na kuomba elimu hiyo isambae hadi vijijini ambako bado kuna uelewa mdogo wa matumizi salama ya gesi ya kupikia.

“Tumejifunza mambo muhimu sana kuhusu usalama wa mitungi yetu na matumizi ya gesi majumbani. Tunaiomba EWURA iende mbali zaidi, hasa vijijini ambako watu bado wana wasiwasi kutumia gesi,” alisema mmoja wa washiriki.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa EWURA kanda ya kati, Bi Hawa Luweno, alisema kuwa semina hiyo ni sehemu ya jitihada za mamlaka hiyo kuhakikisha wananchi wanatumia nishati safi kwa usalama, huku wakielewa haki na wajibu wao kama watumiaji.

“Tulikuja kusikiliza maoni yao, kuzijua changamoto, na kuwapa elimu inayotakiwa ili waendelee kutumia gesi kwa usalama,” alisema Bi Luweno.

EWURA imeahidi kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu matumizi salama ya nishati, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kitaifa wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi kwa ajili ya afya ya jamii na uhifadhi wa mazingira.

 







Tuandikie Maoni Yako Hapa

Post a Comment

0 Comments